WELCOME TO TANZANIA NATIONAL ASSEMBLY OFFICIAL BLOG: CONTACT US: P.O.BOX 941 DODOMA, TANZANIA, WEBSITE: parliament.go.tz , FIND US ON FACEBOOK >>> www.facebook.com/bungetz1, FOLLOW US ON TWITTER >>> @bunge_tz.>>>KARIBUNI

Thursday, August 29, 2019

SPIKA WA BARAZA LA WAWAKILISHI AKAGUA MAANDALIZI YA MKUTANO WA CPA



Spika wa Bunge la Baraza la Wawakilishi Mheshimiwa Zubeir Ali Maulid amewataka Wazanzibari na Watanzania kwa ujumla kutumia fursa waliyoipata ya kuwa wenyeji wa  Mkutano wa 50 wa Mabunge ya Jumuiya ya Madola (CPA), Kanda ya Afrika kujitangaza kibiashara na kitalii.

Mheshimiwa Maulid ametoa rai hiyo leo Kisiwani Zanzibar wakati akikagua maandalizi ya Mkutano huo unaotarajiwa kufanyika kuanzia tarehe 30 Agosti hadi septemba 5 mwaka huu katika Hoteli ya Madinat Al Bahr Business & Spa.

Alisema mkutano huo kufanyika Zanzibar utafungua fursa katika sekta za biashara ikiwemo utalii na kuwataka Watanzania kuonyesha ukarimu kwa wageni hao.

“Tuonyeshe ukarimu wakati kupokea wageni hawa, tuitendee haki nchi yetu, tukikaa nao vizuri wageni wetu itatosha kwa sisi kujitangaza, tutumie fursa hii kwa kadri tutakavyoona inaweza kuisaidia nchi” alisema.

Alisema mkutano huo ni wa kihistoria kwa kuwa unaweza kuvunja rekodi ya mahudhurio ya wajumbe zaidi ya 400 kutoka nchi 18 wanachama ambao unajumuisha maspika, manaibu spika na wabunge.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa CPA, Tawi la Zanzibar, Mheshimiwa Simai Mohammed Said alisema mkutano huo mbali na kutoa fursa za kiuchumi lakini pia utawezesha wajumbe kubadilishana uzoefu wa jinsi ya kutekeleza majukumu yao ikiwemo kuisimamia Serikali katika mambo yanayogusa wananchi.

Awali akizungumzia maandalizi ya awali, Katibu Msaidizi wa CPA, Kanda ya Afrika, Said Yakubu alisema Nchi zote 18 wanachama zimethibitisha ushiriki na kwamba maspika 23 kutoka mabunge makubwa na madogo watahudhuria.

Alisema nchi wanachama wa CPA, Kanda ya Afrika ni Botswana, Cameroon, Eswatini, Ghana, Kenya, Lesotho, Malawi, Mauritius, Msumbiji, Namibia, Nigeria, Rwanda, Seychelles, Siera – Leone, Afrika ya Kusini, Tanzania, Uganda na Zambia.



No comments:

Post a Comment