WELCOME TO TANZANIA NATIONAL ASSEMBLY OFFICIAL BLOG: CONTACT US: P.O.BOX 941 DODOMA, TANZANIA, WEBSITE: parliament.go.tz , FIND US ON FACEBOOK >>> www.facebook.com/bungetz1, FOLLOW US ON TWITTER >>> @bunge_tz.>>>KARIBUNI

Wednesday, October 26, 2016

CAG AAGIZWA KUCHUNGUZA SH. BILIONI 440 ZILIZOWEKWA NA TPA KWENYE MABENKI



Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) imemuagiza Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kufanya ukaguzi maalum katika akaunti zilizofunguliwa kwenye benki mbalimbali za muda maalum (fixed) za Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), zenye thamani ya Sh bilioni 440 zilizofunguliwa na riba ndogo.

Agizo hilo lilitolea mjini Dodoma na Kamati hiyo, wakati ilipomaliza kupitia na kujadili hesabu za mamlaka hiyo za mwaka wa fedha 2014/15.

Mwenyekiti wa kamati hiyo, Mheshimiwa Naghenjwa Kaboyoka, (Mb) amesema katika ukaguzi wa mwaka ujao, CAG anatakiwa ashirikiane na Benki Kuu ya Tanzana (BoT) na Kitengo cha Uchunguzi wa Fedha na kubainisha kiasi cha riba kilichokubaliwa na faida iliyopatikana.

Mheshimiwa Kaboyoka alizitaja benki zilizofunguliwa akaunti hizo na TPA kuwa ni NMB, CRDB, Standard Charter na NBC.

Agizo hilo la kamati limetokana na michango ya wajumbe wa kamati hiyo wakati wa kujadili hesabu za TPA zilizokaguliwa na CAG na kubainika kuwepo kwa akaunti hizo lakini zikiwa zimefunguliwa kwa riba ndogo tofauti na kiwango cha fedha hizo.

Mheshimiwa Kaboyoka, alisema kiasi hicho cha fedha ni kikubwa na kutokana na riba hiyo ndogo TPA imepoteza mabilioni ya fedha, hivyo ni vyema ufanyike uchunguzi ili kubaini kwanini benki hizo zimetoa riba hiyo ndogo kwa kiasi kikubwa cha fedha hizo.

Awali, wakati akichangia katika mjadala wa kamati hiyo, Mbunge wa Msalala Mheshimiwa Ezekiel Maige aliufafanisha ufisadi wa akaunti hizo kama ule wa Kishapu wa jumla ya Sh bilioni tano ambao baada ya kusimamiwa ipasavyo fedha hizo zilipatikana.

“Kwa sasa wastani wa chini viwango vya riba ni asilimia 7.5 na kiwango hicho huongezeka kutokana na kiasi cha fedha ambacho mteja anaweka kwenye akaunti, Kimsingi TPA imepoteza zaidi ya Sh bilioni 32, kwa makusudi kabisa na hii ni motive ya kifisadi,”alidai Mheshimiwa Maige.

Kwa upande wa Mbunge wa Magomeni Mheshimiwa Jamal Kassim Ally alishauri uchunguzi huo uihusishe na BOT kwa kuwa ndio msimamizi wa taasisi za benki nchini na kuhakikisha hatua za kisheria zinachukuliwa dhidi ya wote walioshiriki kuiba fedha hizo.

Naye Mheshimiwa Aeshi Hilal, alisisitiza kuwa pamoja na uchunguzi wa sakata hilo, lazima benki zote zilizohusika na wizi huo wa fedha kupitia riba, nazo ziwajibishwe kwa kuhakikisha kiasi hicho cha fedha kilichopotea kinarejeshwa TPA.

Alisema katika uchunguzi huo wa CAG pia ubainishe ilikuaje hadi benki hizo na TPA zikaingia mkataba wa riba ndogo wa kiasi hicho kikubwa cha fedha tofauti na sheria za fedha.

Pamoja na hoja hiyo, wajumbe wa kamati hiyo pia walizungumzia tatizo la matumizi makubwa ya mamlaka hiyo ya bandari wakati imekuwa ikichangia kiasi kidogo kwa upande wa gawio la serikali.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TPA Deusdedit Kakoko alikiri kuwepo kwa tatizo hilo la akaunti na kubainisha kuwa lilitokea katika utawala wa nyuma huku akisisitiza kutekeleza maagizo ya serikali katika kutafutia ufumbuzi jambo hilo.

Kuhusu matumizi ya mamlaka hiyo, alisema tayari TPA imeanza kudhibiti matumizi yake na kutolea mfano kuwa inaweza kupunguza kutoka matumizi ya Sh bilioni 478 hadi kufikia Sh bilioni 200.

Naye Msajili wa Hazina, Lawrence Mafuru alisema tayari mamlaka hiyo imeanza kufanya vizuri katika eneo la gawio kwa serikali kwani katika kipindi kifupi tangu bodi mpya ianze utendaji, mamlaka hiyo imechangia serikalini kiasi cha Sh bilioni 150 kutoka Sh bilioni 12 za nyuma.


Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) wakipitia na kujadili Hesabu za mamlaka ya Bandari Nchini (TPA) hiyo za mwaka wa fedha 2014/15.

Mwenyekiti wa kamati ya PAC, Mheshimiwa Naghenjwa Kaboyoka katikati akisisitiza jambo wakati kamati yake ilipokutana na watendaji wa TPA, kupitia na kujadili hesabu za malka hiyo za mwaka 2014/15. Kushoto ni Makamu mwenyekiti wa kamati hiyo,Mheshimiwa Aeshi Hillal

Mkurugenzi mkuu wa mamlaka ya bandari nchini TPA, Deusdedit Kakoko akitolea ufafanuzi hoja mbalimbali zilizoibuliwa na wajumbe wa kamati ya PAC, katika kikao cha kamati hiyo mjini Dodoma

Msajili wa Hazina, Lawrence Mafuru akieleza jambo kaika kikao cha Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) wakipitia na kujadili Hesabu za mamlaka ya Bandari Nchini (TPA) hiyo za mwaka wa fedha 2014/15.

No comments:

Post a Comment